MFUMO WA e-DELIVERY WAANZA RASMI
Tume ya Taifa ya Mipango imeanza rasmi kutumia mfumo mpya wa Kitaifa wa kusimamia Mipango na Miradi ya Maendeleo wa e-Delivery System kuanzia Julai Mosi 2026
Hayo yamebainishwa na Naibu Katibu Mtendaji – kutoka Tume anayesimamia masuala ya Menejimenti ya Utendaji na Tathmini Bw. Sosthenes Kewe Jijini Arusha katika awamu ya nne ya mafunzo ya mfumo huo, kwa maafisa kutoka Idara za Mipango, Sera, Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara za Kisekta, Sekretariet za Mikoa, na Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Amesema mfumo huo wa kieletroniki ndiyo mfumo pekee nchini utakaotumika katika masuala yote ya uibuaji, uidhinishaji, utekelezaji, ufuatiliaji na tathmini ya miradi yote ya maendeleo itakayotekelezwa kuanzia ngazi ya taasisi na Halmashauri ili kuhakikisha inaendana na Malengo ya Dira 2050 pamoja na vipaumbele vingine ya Kitaifa.
Pia Bw Kewe amebainisha kuwa hadi sasa Tume ya Taifa ya Mipango imeshatoa mafunzo kwa maafisa zaidi ya 1200 na wataendelea kutoa kwa makundi mengine yanayohusika wakiwemo viongozi ili kuhakikisha wahusika wote wanaelewa mfumo huo ipasavyo.